Kombe la Dunia 2026 linaanza lini, na maswali mengine kuhusu Kombe la Dunia la kwanza lenye timu 48

Chanzo cha picha, Getty Images
Siku za kuelekea Kombe la Dunia la 2026 zi karibu, mashindano ambayo yatakuwa na timu 48 zinazoshiriki na zaidi ya mechi 100 kwa mara ya kwanza katika historia yake.
Michuano ya 23 ya Kombe la Dunia itafanyika nchini Marekani, Mexico na Canada kuanzia tarehe 11 Juni hadi 19 Julai.
Idadi ya rekodi ya timu 48, ambazo ni 16 zaidi ya zilizoshiriki Qatar miaka minne iliyopita, zitakuwa zikishindania kombe la 2026.
Hii inafanya mashindano haya kuwa makubwa zaidi katika historia, na kuongeza idadi ya mechi hadi 104, ambazo zitachezwa kwa mara ya kwanza katika nchi tatu tofauti.
Huu ni muhtasari wa kile unachohitaji kujua kuhusu Kombe la Dunia litakalofanyika Amerika Kaskazini.
Makundi 12 ya Kombe la Dunia la 2026
Mashindano haya ya FIFA World Cup 2026 yatakuwa na mfumo mpya unaojumuisha makundi 12 yenye timu 4 kila moja.
Timu mbili za juu kutoka kila kundi kati ya makundi 12, pamoja na timu nane bora zilizoshika nafasi ya tatu, zitafuzu kwenda hatua ya mtoano.
Kwa upande wa kuchagua timu bora za nafasi ya tatu, timu zitapimwa kwa vigezo vifuatavyo:
Idadi ya alama walizokusanya
Tofauti ya mabao (mabao yaliyofungwa dhidi ya yaliyofungwa)
Idadi ya mabao yaliyofungwa
Hivyo, vigezo hivi vitatumika kama msingi wa kuamua ni timu zipi za nafasi ya tatu zitakazofuzu kwenda hatua ya mwisho ya mashindano.

Chanzo cha picha, Jim WATSON/AFP via Getty Images
Michuano itakuwa lini?
Michuano hii itafanyika kati ya 11 Juni hadi 19 Julai, ikiwa na muda wa rekodi wa siku 39, yaani siku 10 zaidi ya Kombe la Dunia la Qatar, na zaidi ya siku za mashindano ya 2014 na 2018.
Sherehe ya ufunguzi zitafanyika Alhamisi, 11 Juni katika uwanja wa kihistoria wa Estadio Azteca, na mechi ya ufunguzi itakuwa kati ya Mexico na Afrika Kusini.
Kwa jumla kutakuwa na mechi 72 za hatua ya makundi zitakazochezwa ndani ya siku 17, kuanzia ufunguzi hadi Jumamosi 27 Juni.

Chanzo cha picha, Getty Images
Michuano itafanyika wapi?
FIFA World Cup 2026 itafanyika kwa mara ya kwanza katika miji 16 ndani ya nchi tatu, ambapo:
Miji 11 iko Marekani, miji mitatu Mexico na miji miwili Canada.
Kwa kuwa FIFA inaweka vikwazo vya majina ya kibiashara ya viwanja vilivyokuwepo awali, kwa Kombe la Dunia la 2026, viwanja hivyo vitaitwa kwa jina la jiji mwenyeji.
Huko Mexico, sherehe za ufunguzi zitafanyika katika Uwanja wa Jiji la Mexico, uwanja ambao utaweka historia kuwa wa kwanza kuandaa michuano mitatu ya Kombe la Dunia, na pia huko Guadalajara na Monterrey.
Huko Canada kuna maeneo mawili: Toronto na Vancouver.
Marekani itakuwa mwenyeji mkuu wa michuano hii: Atlanta, Boston, Dallas, Houston, Kansas City, Los Angeles, Miami, New York/New Jersey, Philadelphia, San Francisco/Santa Clara na Seattle.

Chanzo cha picha, Getty Images
Timu pendwa zinazotajwa

Chanzo cha picha, Getty Images
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Timu ya Hispania, mabingwa wa Ulaya, ndiyo inayopewa nafasi kubwa ya kushinda Kombe la Dunia la 2026, baada ya kukamilisha awamu ya kufuzu bila dosari yoyote.
Kikosi chao kimejaa vipaji, huku wachezaji kama Pedri, Fabián Ruiz, Martín Zubimendi, Rodri, mshindi wa Ballon d'Or ya 2024 na Lamine Yamal, mmoja wa wachezaji bora wa mpira wa miguu duniani.
Baada tu ya Hispania, kizazi cha sasa cha wachezaji wa Uingereza kinatarajiwa kutamani taji hilo, baada ya kumaliza kama washindi wa pili katika Mashindano mawili ya mwisho ya Ulaya.
Kikosi cha Uingereza cha Thomas Tuchel kilifuzu Kombe la Dunia kikiwa na rekodi nzuri, kikishinda mechi zao zote bila kuruhusu bao. Wanajivunia kikosi kilichojaa majina makubwa, wakiwemo Jude Bellingham na Harry Kane.
Ufaransa pia ni mshindani mkubwa. Timu ya Didier Deschamps inajivunia safu ya ushambuliaji imara, ikiwa na Michael Olise, Kylian Mbappé, na Ousmane Dembélé, mshindi wa sasa wa Ballon d'Or. Washindi wa pili wa mwaka 2022 walimaliza bila kushindwa katika raundi za kufuzu za Ulaya.
Argentina, mabingwa wa dunia wanaotawala, walishinda kundi lao la kufuzu la Amerika Kusini kwa tofauti kubwa, wakimaliza pointi tisa mbele ya Ecuador iliyoshika nafasi ya pili. Wakiwa na mataji mawili ya Copa América na Kombe la Dunia moja waliloshinda katika miaka minne tu, Albiceleste ni wapinzani wazuri.

Chanzo cha picha, Getty Images
Norway haijashiriki Kombe la Dunia tangu mwaka 1998 na haijawahi kufika zaidi ya hatua ya 16 bora. Hata hivyo, ikiwa na nyota wa Manchester City Erling Haaland, aliyefunga mabao 16 katika hatua za kufuzu, inaweza kuleta mshangao mkubwa.
Kampeni yao ya kufuzu ilikuwa kamilifu, wakishinda mechi zote nane walizocheza, ikiwemo ushindi wa nyumbani na ugenini dhidi ya mabingwa wa dunia mara nne, Italia.
Morocco nayo ilikuwa timu nyingine iliyoshinda mechi zake zote za kufuzu na kwa sasa ipo nafasi ya nane duniani. Walifika fainali ya AFCON ya mwaka huu na, licha ya kufungwa 1-0 na Senegal, walitunukiwa ubingwa katika mazingira yaliyozua utata. Huenda wakawa na matumaini makubwa ya kusonga mbele kutoka kundi lenye Brazil, Scotland, na Haiti.
Misri, ikiwa na Mohamed Salah katika kikosi chake, pia ina matumaini ya kufuzu kutoka kundi linalojumuisha Ubelgiji, New Zealand, na Iran.
Japan ndiyo timu yenye nguvu zaidi barani Asia na ilipita kirahisi katika hatua za kufuzu, ikiruhusu mabao matatu pekee katika mechi 16. Pia walipata ushindi wao wa kwanza kabisa dhidi ya England kwa kuifunga 1-0 katika mechi ya kirafiki iliyochezwa Wembley mwishoni mwa Machi. Watakutana na Uholanzi, Tunisia, na Sweden.
Colombia ina imani ya kufanya vizuri baada ya kampeni nzuri ya kufuzu kutoka Amerika Kusini ambapo waliifunga Brazil na Argentina na kumaliza katika nafasi ya tatu kwa ujumla.
Na vipi kuhusu wenyeji wa mashindano? Canada, katika ushiriki wake wa tatu, inaweza pia kuleta mshangao. Imepoteza mechi zake zote sita za awali za Kombe la Dunia, lakini imepangwa katika kundi linaloonekana kuwa nafuu dhidi ya Qatar, Switzerland, na Bosnia-Herzegovina.

Chanzo cha picha, Getty Images
Timu zinazoshiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza
Nchi nne zitashiriki michuano ya kombe la dunia kwa mara ya kwanza.
Kisiwa kidogo cha Karibiani cha Curaçao kitakuwa nchi ndogo zaidi kuwahi kushiriki Kombe la Dunia, kikiwa na wakazi wapatao 150,000 na eneo la kilomita za mraba 444. Kitakutana na Ujerumani, Ivory Coast, na Ecuador katika Kundi E.
Wakati huo huo, Cape Verde ndiyo taifa la tatu kwa udogo kufuzu kwa Kombe la Dunia baada ya Curaçao na Iceland. Ni visiwa 10 vilivyopo katika Bahari ya Atlantiki vyenye idadi ya watu chini ya 525,000. Watacheza dhidi ya Hispania, Saudi Arabia, na Uruguay katika Kundi H.
Pia kuna timu mbili zinazoshiriki kwa mara ya kwanza kutoka Asia: Uzbekistan na Jordan.
Wauzbekistan, ambao walifika nusu fainali ya AFC Asian Cup mwaka 2011, walisubiri kwa muda mrefu kufuzu chini ya kocha Fabio Cannavaro, nahodha wa timu ya Italia iliyoshinda Kombe la Dunia mwaka 2006.
Timu hiyo inayojulikana kama White Wolves ina wachezaji kama beki wa Manchester City Abdukodir Khusanov na mshambuliaji wa zamani wa AS Roma Eldor Shomurodov, na wanatarajia kufanya vizuri katika kundi linalojumuisha Ureno, Colombia, na Jamhuri ya Demokrasia ya Congo.

Chanzo cha picha, Getty Images
Jordan, kwa upande mwingine, ilimaliza nyuma ya Korea Kusini baada ya kupata ushindi mara nne na sare nne katika mechi 10 za raundi ya tatu ya kufuzu kwa timu za Asia.
Kwa sasa Jordan ipo nafasi ya 64 duniani, na maendeleo yao yamekuwa ya taratibu lakini thabiti. Walifika fainali ya AFC Asian Cup ya mwaka 2023, ambapo walifungwa na wenyeji Qatar. Katika Kundi J, watakutana na Argentina, Algeria, na Austria.
Kombe hili la Dunia litakuwa na mfumo mpya wenye makundi 12, kila kundi likiwa na timu nne.
Timu mbili za juu kutoka kila kundi kati ya hayo 12 pamoja na timu nane bora zilizomaliza nafasi ya tatu zitafuzu kwenda hatua ya mtoano, itakayoanza na hatua ya timu 32 bora.














