Moja kwa moja, Iran yasema itawazuia wakaguzi wa nyuklia kukagua vituo vyake vilivyoshambuliwa

Kauli hiyo imekuja wakati Qatar ikitangaza kumalizika kwa duru nyingine ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kati ya Iran na Marekani yaliyofanyika mjini Doha.

Skip Video and continue reading
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Mariam Mjahid na Lizzy Masinga

  1. Pape Gueye asusa kuichezea Senegal hadi benchi la ufundi litakapobadilishwa

    Gueye

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kiungo wa Senegal, Pape Gueye, amesema kuwa atasitisha kwa muda kuichezea timu ya taifa kwa muda wote ambao benchi la ufundi la sasa litaendelea kuiongoza timu hiyo.

    Uamuzi wa mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 unafuatia kuondolewa kwa Senegal katika hatua ya 32 bora ya Kombe la Dunia, baada ya kupoteza kwa kufungwa na Ubelgiji kwa mabao 3-2 chini ya kocha Pape Thiaw.

    Habib Diarra na Ismaïla Sarr waliifungia Senegal mabao mawili yaliyoiweka mbele, lakini mabao ya dakika za mwisho kutoka kwa Romelu Lukaku na Youri Tielemans yalipeleka mchezo huo katika muda wa nyongeza.

    Belgium ilipewa penalti yenye utata katika dakika ya 125, na Tielemans akafunga mkwaju huo wa penalti na kuitupa Senegal nje ya mashindano.

    Gueye, anayekipiga katika klabu ya Villarreal CF nchini Hispania, alianza mchezo huo lakini alitolewa dakika ya 66 na nafasi yake kuchukuliwa na Lamine Camara.

    Kupitia mitandao ya kijamii, Gueye alisema:

    "Nitarejea baadaye kuzungumzia kuondolewa kwetu... lakini leo natangaza kwamba mradi tu benchi hili la ufundi litaendelea kuwepo, nitakuwa napumzika kuichezea timu ya taifa."

    Gueye ameichezea Senegal mechi 45 na amefunga mabao mawili, yakiwemo yale aliyofunga katika ushindi wa hatua ya makundi dhidi ya Iraq.

    Unaweza kusoma;

  2. Maafisa wa afya Gaza watangaza hali mbaya ya upatikanaji wa tiba kwa majeruhi

    Hasira ya umma imeongezeka katika nchi nyingi kote ulimwenguni kutokana na athari za kibinadamu za vita dhidi ya watu wa Gaza

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maafisa wa afya katika ukanda wa Gaza wanasema kuwa watu 15,000 waliojeruhiwa au wanaougua magonjwa makubwa kutokana na vita hawapati matibabu wanayohitaji, huku watu 300 wakidaiwa kufariki dunia walipokuwa wakisubiri kuhamishiwa nje ya Gaza kwa ajili ya matibabu.

    Kwa kawaida, nchi zinazowapokea wagonjwa huwa na vigezo maalumu vya kuwaruhusu kuingia, na wagonjwa hulazimika kupitia hatua kadhaa za ukaguzi wa kiusalama, ikiwemo ukaguzi unaofanywa na Israel, kabla ya kuondoka Gaza.

    Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, kati ya zaidi ya vituo 600 vya afya vilivyopo Gaza, ni takriban vituo 30 pekee vinavyofanya kazi kikamilifu.

    Mashirika ya misaada yanasema Israel inaendelea kuweka vikwazo katika uwasilishaji wa dawa na vifaa muhimu vya matibabu kwenda Gaza, madai ambayo Israel imeyakanusha.

    Unaweza kusoma;

  3. Watu wasiopungua 13 wameuawa katika 'shambulio kubwa zaidi' la Urusi mjini Kyiv

    Milipuko ilitengeneza shimo kubwa karibu na majengo yaliyoharibiwa kwa mabomu mjini Kyiv

    Chanzo cha picha, Reuters

    Wanajeshi wa Urusi wamefanya mashambulizi makubwa ya droni na makombora dhidi ya Kyiv usiku kucha, na kusababisha vifo vya watu 13, katika kile ambacho meya wa jiji hilo amekielezea kuwa "shambulio kubwa zaidi kuwahi kulenga mji mkuu wa Ukraine."

    Vitali Klitschko ametangaza Ijumaa kuwa siku ya maombolezo na kusema kuwa takriban watu 90 wamejeruhiwa. Pia alisema kuwa kituo cha magari ya wagonjwa ni miongoni mwa maeneo yaliyopigwa na mashambulizi hayo.

    Ingawa mashambulizi mengine ya awali yalisababisha vifo vingi zaidi au yalihusisha matumizi ya silaha nyingi zaidi, mashambulizi haya ya karibuni yalilenga maeneo mengi katika sehemu mbalimbali za Kyiv kwa wakati mmoja.

    Vitongoji kadhaa vililazimika kuhamishwa huku milipuko ikitikisa majengo kote jijini, saa chache baada ya Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy, kuonya kuwa Urusi ilikuwa ikijiandaa kufanya shambulio.

    Unaweza kusoma;

  4. Christian Brothers yaruhusiwa kusitisha kwa muda malipo ya fidia kwa waathiriwa wa unyanyasaji nchini Australia

    Tawi la Oceania la Congregation of Christian Brothers linataka kuuza mali zake ili kupata fedha za kulipa sehemu ya fidia kwa waathiriwa

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mahakama ya Australia imeipa taasisi ya kidini ya Congregation of Christian Brothers muda wa kusitisha kwa muda malipo ya fidia kwa waathiriwa wa unyanyasaji wa kingono dhidi ya watoto, baada ya taasisi hiyo kudai kuwa imeanza kuishiwa fedha za kulipa mamilioni ya dola.

    Taasisi hiyo iliieleza mahakama kuwa inakabiliwa na hali mbaya ya kifedha na inapanga kuuza mali zake zilizobaki ili kupata fedha za kulipa sehemu ya fidia.

    Pia iliomba kusimamishwa kwa muda kwa malipo hayo ili kuwapa waathiriwa nafasi ya kuzingatia mpango huo wa malipo, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Australia.

    Kundi hilo linakadiria kuwa linadaiwa kulipa waathiriwa dola za Australia milioni 774 (sawa na dola za Marekani milioni 534 au pauni milioni 400), kiasi kinachozidi fedha taslimu ilizonazo za dola milioni 23 pamoja na mali zenye thamani ya dola milioni 216.

    Likiwa limeanzishwa nchini Ireland, shirika la Christian Brothers limeendesha shule na vituo vya kulelea watoto yatima nchini Australia na New Zealand tangu miaka ya 1850.

    Kwa mujibu wa tovuti yake, shughuli za tawi lake la Oceania zinahusisha elimu ya watu wazima, shughuli za haki za kijamii kwa wakimbizi, waomba hifadhi, jamii za asili na vijana walio katika mazingira magumu.

    Hata hivyo, uchunguzi umebaini kuwa shule na vituo vya watoto yatima vinavyoendeshwa na Christian Brothers vimekuwa maeneo ya unyanyasaji mkubwa wa kingono dhidi ya watoto tangu miaka ya 1950.

    Mwaka 2013, tume iliyochunguza namna taasisi zilivyoshughulikia visa vya unyanyasaji wa kingono dhidi ya watoto ilihitimisha kuwa Christian Brothers "ilishindwa kabisa kuwalinda watoto walio katika mazingira hatarishi waliokuwa chini ya uangalizi wake", huku baadhi ya wanachama wake baadaye wakipatikana na hatia ya makosa ya unyanyasaji wa kingono.

    Tume hiyo pia ilibaini kuwa viongozi wa taasisi hiyo walikuwa wanafahamu kuhusu vitendo hivyo vya unyanyasaji lakini hawakuchukua hatua za kuvikomesha.

    Unaweza kusoma;

  5. Vance: Trump hana nia ya kuishambulia tena Iran bila sababu za msingi

    G

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, amesema Rais Donald Trump hana nia ya kuanzisha tena operesheni za kijeshi dhidi ya Iran bila kuwa na lengo lililo wazi na maalumu.

    Akizungumza na waandishi wa habari Jumatano, Vance alisema, "Ninachoweza kuthibitisha ni kwamba Rais Trump hana nia ya kuwarejesha wanajeshi wetu huko isipokuwa pale ambapo itakuwa lazima kabisa kufanya hivyo."

    Makamu huyo wa Rais alionya kuwa jaribio lolote la Iran kufufua mpango wake wa nyuklia au kuhatarisha usafirishaji wa kibiashara baharini linaweza kuilazimisha Washington kubadili mkakati wake.

    Vance pia alithibitisha kuwa mazungumzo yanayoendelea mjini Doha "yanapiga hatua vizuri" na kusisitiza kuwa utawala wa Marekani unaendelea kushiriki katika mazungumzo hayo "kwa nia njema."

    Unaweza kusoma;

  6. Nigeria yataka kufidiwa kwa mali za raia wake waliokimbia Afrika Kusini

    h

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Nigeria imesema itaitaka Afrika Kusini kulipa fidia kwa mali na biashara zilizoachwa na raia wake waliokimbia nchi hiyo kutokana na maandamano yaliyowalenga wahamiaji wasio na nyaraka.

    "Suala hili litajadiliwa kati ya serikali mbili katika ngazi za juu zaidi," alisema msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Nigeria, Kimiebi Imomotimi Ebienfa.

    Kaimu Balozi Mkuu wa Nigeria nchini Afrika Kusini, Alexander Ajayi, alisema kupitia televisheni ya nchini humo Jumanne kuwa serikali imeanza kuorodhesha biashara na mali zilizoachwa na Wanigeria.

    Mfanyabiashara mmoja wa Nigeria anayesubiri kurejeshwa nyumbani aliiambia BBC kwamba alikuwa ameishi Afrika Kusini kwa karibu muongo mmoja na ameacha biashara yake na nyumba yake kwa sababu aliogopa usalama wake.

    Oghodero Erejor Wilson, mwenye umri wa miaka 32, alisema amepoteza "kila kitu kwa sababu ya hofu".

    "Nimeacha kila kitu nyumbani kwangu, hata nguo zangu," alisema.

    Yeye ni miongoni mwa mamia ya Wanigeria ambao bado wanasubiri kuondolewa kutoka Afrika Kusini.

    Zaidi ya Wanigeria 600 tayari wamerejeshwa nchini mwao katika wiki za karibuni.

    Hata hivyo, Mamlaka za Afrika Kusini zinasema wale waliosafirishwa kurejea nyumbani walikuwa nchini humo kinyume cha sheria, ingawa Nigeria inapinga madai hayo.

    Unaweza kusoma;

  7. Iran yasema itawazuia wakaguzi wa nyuklia kukagua vituo vyake vilivyoshambuliwa

    j

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Baqer Qalibaf, amesema wakaguzi wa Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki (IAEA) hawataruhusiwa kuingia katika vituo vya nyuklia vya Iran vilivyoharibiwa na mashambulizi.

    "Kwa mujibu wa sheria iliyopitishwa na Bunge na kuidhinishwa na Baraza Kuu la Usalama wa Taifa, hakuna mazingira yatakayoruhusu ufikiaji wa maeneo yaliyoshambuliwa na kuharibiwa," alisema Qalibaf.

    Kauli hiyo imekuja wakati Qatar ikitangaza kumalizika kwa duru nyingine ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kati ya Iran na Marekani yaliyofanyika mjini Doha.

    Unaweza kusoma;

  8. Mashambulizi ya makombora na droni za Urusi mjini Kyiv yaua watu 10

    f

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Takriban watu 10 wameuawa katika mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani ya Urusi dhidi ya mji mkuu wa Ukraine, Kyiv, usiku wa kuamkia Alhamisi.

    Milipuko zaidi ya kumi ilisikika katika maeneo ya kati na mashariki mwa Kyiv, huku wakazi wakikimbilia vituo vya metro vilivyotumika kama makazi ya kujikinga.

    Meya wa Kyiv alisema kupitia Telegram kuwa mji huo ulikuwa ukishambuliwa kwa makombora ya balestiki na droni, huku milipuko ikisikika katika sehemu mbalimbali za jiji.

    Mashambulizi hayo yalifuatia onyo la Jeshi la Anga la Ukraine kuhusu makombora ya balestiki yaliyokuwa yakielekea mji mkuu.

    Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, alifupisha ziara yake nchini Ireland Jumatano baada ya kupokea taarifa za kijasusi kwamba Urusi ilikuwa ikijiandaa kufanya shambulio jipya dhidi ya nchi yake.

    "Nawasihi wananchi kuwa waangalifu sana, wawalinde watoto na familia zao, na wakimbilie kwenye makazi ya kujikinga," Zelensky alisema katika mkutano na waandishi wa habari.

    Aliongeza kuwa Urusi imekuwa ikijiandaa kwa muda mrefu kutekeleza shambulio hilo kubwa dhidi ya Ukraine.

    Urusi imeendelea kushambulia miji ya Ukraine, ikiwemo Kyiv, kwa makombora na ndege zisizo na rubani tangu ilipoanzisha uvamizi wake wa kijeshi nchini humo mwezi Februari mwaka 2022.

    Unaweza kusoma:

  9. Zaidi ya watu 900 wakamatwa katika maandamano dhidi ya wahamiaji Afrika Kusini

    h

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Zaidi ya watu 900 wamekamatwa kufuatia maandamano ya kitaifa dhidi ya wahamiaji yaliyofanyika Jumanne nchini Afrika Kusini, ambayo kwa kiasi kikubwa yalikuwa ya amani lakini katika baadhi ya maeneo yaligeuka kuwa ya vurugu na kusababisha uporaji wa maduka.

    Naibu Kamishna wa Kitaifa wa Polisi, Tebello Mosikili, amesema maandamano 108 kati ya 120 yaliyofanyika nchini yalikuwa ya amani, huku maandamano 12 yakihitaji polisi kuingilia kati.

    Amesema sababu za kukamatwa kwa watu hao zinajumuisha ukiukaji wa sheria za uhamiaji, kufanya vurugu hadharani, kuwaficha wahamiaji wasio na nyaraka halali na wizi.

    Polisi pia wamesema mtu mmoja alipigwa risasi na kuuawa usiku wa Jumanne katika kitongoji cha Alexandra, mjini Johannesburg, ambako wakazi walikuwa wakipora maduka madogo maarufu kama spaza shops yanayomilikiwa na raia wa kigeni.

    Mamlaka zilisambaza askari wa ziada katika majimbo matano kati ya tisa ya nchi hiyo usiku kucha, huku wanajeshi wakipelekwa katika eneo la Hillbrow katikati mwa Johannesburg, ambako watu wawili walijeruhiwa kwa kupigwa risasi.

    Katika mji wa bandari wa Durban, polisi wameanza uchunguzi kuhusu kifo cha raia mmoja wa kigeni ambaye inadaiwa alijirusha kutoka ghorofa ya nane ya jengo moja usiku kabla ya maandamano, akiamini alikuwa analengwa.

    Maandamano ya Jumanne yaliandaliwa kuashiria mwisho wa muda uliowekwa na kundi linalopinga wahamiaji, lililokuwa limetaka wahamiaji wasiokuwa na vibali halali vyaondoke Afrika Kusini.

    Unaweza kusoma;

  10. Marekani yafikiria kuhamisha wanajeshi wake kutoka Saudi Arabia - Gazeti la Wall Street

    g

    Chanzo cha picha, Reuters

    Kwa mujibu wa gazeti la Wall Street Journal Marekani inatafakari kupunguza au kuhamisha baadhi ya wanajeshi na vifaa vyake vya kijeshi kutoka Saudi Arabia, hatua inayotokana na mvutano unaoongezeka kati ya Washington na Riyadh kuhusu vita vya Iran na usalama wa usafiri wa baharini katika Mlango wa Hormuz.

    Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Saudi Arabia ilikataa kuruhusu matumizi ya baadhi ya kambi zake za kijeshi na anga yake wakati Marekani ilipoanzisha operesheni ya kulinda usafiri wa meli katika Mlango wa Hormuz mapema mwaka huu.

    Hatua hiyo, kwa mujibu wa maafisa wa Marekani waliozungumza na gazeti hilo, iliiweka Washington katika hali ngumu na kuathiri utekelezaji wa operesheni ya kijeshi iliyopewa jina la Project Freedom, ambayo Rais Donald Trump alikuwa ameitangaza kwa lengo la kuhakikisha usalama wa meli zinazopita katika njia hiyo muhimu ya baharini.

    Ripoti hiyo inaongeza kuwa miongoni mwa hatua zinazozingatiwa ni kuhamisha baadhi ya wanajeshi na vifaa vya kijeshi kwenda mataifa kama Israel na Jordan, ambayo Washington inaamini yalishirikiana kwa karibu zaidi wakati wa mzozo na Iran.

    Hata hivyo, Wall Street Journal imesisitiza kuwa hakuna uamuzi wa mwisho uliotolewa kuhusu uwezekano wa kuondolewa kwa wanajeshi wa Marekani kutoka Saudi Arabia, na kwamba kwa sasa suala hilo liko katika hatua ya kutathmini hatua mbalimbali.

    Hadi sasa, maafisa wa Marekani hawajathibitisha wala kukanusha uwezekano wa kuondolewa kwa wanajeshi wao kutoka Saudi Arabia hivi karibuni.

    Unaweza kusoma;

  11. Dakika tatu za maajabu zaiondoa Senegal Kombe la Dunia

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Senegal imeondolewa kwenye Kombe la Dunia 2026 kwa njia ya kusikitisha baada ya kupoteza mabao 3-2 dhidi ya Ubelgiji katika muda wa nyongeza, licha ya kuwa ilikuwa inaongoza kwa mabao mawili hadi dakika za mwisho za mchezo.

    Matokeo hayo yanaifanya Senegal kuwa timu ya tano kutoka Afrika kuaga mashindano hayo, ikiifuata Afrika Kusini, Ivory Coast, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Tunisia.

    Kwa sasa, Morocco ndiyo timu pekee ya Afrika iliyofuzu hatua ya 16 bora baada ya kuwaondoa Uholanzi kwa mikwaju ya penalti.

    Algeria, Misri, Cape Verde na Ghana bado zinasaka nafasi ya kuungana nao.

    Senegal ilianza vyema mechi hiyo ya hatua ya 32 bora mjini Seattle, ikitangulia kwa bao la Habib Diarra dakika ya 25 kabla ya Ismaila Sarr kuongeza la pili dakika ya 51 na kuifanya ionekane kuwa njiani kutinga hatua inayofuata.

    Hata hivyo, ndani ya dakika tatu za mwisho za muda wa kawaida, Belgium ilibadili kabisa mchezo. Romelu Lukaku, aliyeingia akitokea benchi, alifunga dakika ya 86 kabla ya nahodha Youri Tielemans kusawazisha dakika ya 89 na kuupeleka mchezo katika muda wa nyongeza.

    Senegal ilijitahidi kuhimili shinikizo katika muda wa nyongeza, lakini katika dakika ya 120+5, Tielemans alipata penati na kuifunga mwenyewe, akiipa Ubelgiji ushindi wa mabao 3-2 na tiketi ya hatua ya 16 bora.

    Ubelgiji sasa itakutana na Marekani katika hatua ya 16 bora baada ya Wamarekani kuifunga Bosnia na Herzegovina mabao 2-0.

    Unaweza kusoma;

  12. Iran na Marekani zahitimisha mazungumzo Doha bila dalili za amani ya kudumu

    d

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Iran na Marekani zimehitimisha duru nyingine ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja Jumatano bila kuonyesha dalili za kupiga hatua kuelekea makubaliano ya amani ya kudumu, huku mazungumzo yakijikita zaidi katika masuala ambayo pande hizo zilisema yalikuwa tayari yameshughulikiwa chini ya makubaliano ya muda yaliyotangazwa wiki mbili zilizopita.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Qatar imesema hatua chanya zimepatikana katika mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kati ya Iran na Marekani yaliyofanyika mjini Doha, huku pande hizo zikikubaliana kuendeleza mazungumzo baada ya mazishi ya kiongozi wa zamani wa juu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei.

    Soma zaidi:

  13. Hujambo natumai umzima, karibu kwa matangazo ya moja kwa moja.